PAUL NDETEI
1.
Kupendwa kuna mafao,wapendwao mashahidi
Huwa ni furaha kwao,zimiminwapo ahadi
Hufaa walitunzao,kwa uwazi wa fuadi
Mahaba pumbao lao
2.
Penzi halina kituo,pawapo zuri kusudi
Yakini ni ufunguo,wa mema yaso asidi
Hawafunzi kwenye chuo,tangu jadi na jadudi
Mahaba pumbao lao
3.
Mshumaa uwakao,upepo haukaidi
Usipozingwa na hao,huba hubaki miadi
Raha kwao wajengao,penzi pamwe hufaidi
Mahaba pumbao lao
4.
Hayana mkali ‘wao’,popote hubisha hodi
Halichelei komoo,uongo unapozidi
Ovyo haliitwi ‘njoo’,kiranga hukikaidi
Mahaba pumbao lao
5.
Ni la wawili ambao,kawajalia Wadudi
Ndilo zela radhi zao,lisojazwa mazidadi
Viapo vyake ni ‘ndio’,ya mtima kuahidi
Mahaba pumbao lao
6.
Beti tandatu mgao,pokeeni ni zawadi
Na nduzangu mtungao,sitaki kuki la ngwidi
Utungo wasema nao,nyonda wa mja wahedi
Mahaba pumbao lao
© PAUL NDETEI
© MSHAIRI MSI SHARI
NAIROBI-🇰🇪❤️