Wanjohi. P. Mugambi
Malenga Kitunguu Machoni
Nairobi Kenya
Mwambie nilipo leo, si pale nilipokuwa
Yamegeuka ya leo, mengine yameshakuwa
Sicho kile kichocheo, mtima kilichouwa
Mwambie!
Mwambie letu eneo, si hivyo lilivyokuwa
Leo linao noleo, lanoa bongo visawa
Hakuna mapendeleo, jinsi yalivyokuwa
Mwambie!
Mwambie nilipo leo, kwake nipofukuziwa
Mwana lipata pepeo, faudi kutuliziwa
Nitatulia tokeo, mi’ nilipochukuliwa
Mwambie!
Mwambie na mwelekeo, ule wa kutarikiwa
Alochukuwa macheo, wazimu mimi nikawa
Na lipofika machweo, kubadili kutokuwa
Mwambie!
Mwambie kwalo komeo, moyo ulivyochukiwa
Na chuki ilivyo leo, nimekubali fanyiwa
Kiwe kikali kinyweo, bado maji yatanywewa
Mwambie!
Mwambie cha matokeo, kile kilikataliwa
Ndicho chanipa chocheo, hatua kuegemewa
Kwani kuna marejeo, kurudi yasiyojuwa
Mwambie!

