Wewe usiyenitaka, kuniona hadharani,
Kisa chuki umeweka, wanidharuliani?
Mimi nisiye na shaka, nina zangu hamkani,
Mwenye roho ya korosho, je unafaidi nini?
Wewe mvimbisha kichwa, ninazungumza nawe,
Acha kujifanya mchwa, kuniona mimi jiwe,
Unadhani nimeachwa, sababu siendi nawe?
Mwenye roho ya korosho, je unafaidi nini?
Wewe wajifanya bubu, nia yako iko wazi,
Kweli ulinighilibu, ndipo ukapande ngazi,
Sasa utapata tabu, kama ndiyo yako kazi,
Mwenye roho ya korosho, je unafaidi nini?
Wewe hata huna haya, unachofanya si sawa,
Ndiyo ya kwako tabiya, tangu ulipozaliwa,
Kizuri kwako kibaya, husiti kukichukuwa,
Mwenye roho ya korosho, je unafaidi nini?
Mtunzi: Alfred Lobawoi
Mahali: Ruiru

